Utanzia katika kasida za Kiswahili: Mifano kutoka mkoa wa Mjini Magharibi Unguja
Loading...
Date
2016
Authors
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
Chuo Kikuu cha Dodoma
Abstract
Utafiti huu ulilenga kuchunguza utanzia katika Kasida za Kiswahili kwa kutumia
mifano kutoka Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja. Dhana ya utanzia katika tasnifu
hii ina maana ya maneno au mazingira yanayozua huzuni, jitimai, majonzi,
masikitiko, majuto na maumivu ya mwili, roho au akili kwa hadhira. Utanzia
unajengwa na vipengele kama vile, vifo, ajali, vifungo, mabalaa, ulemavu, vilio,
maradhi, njaa na mateso. Yumkini, hakuna uchunguzi wa kutosha kuhusu utanzia
katika kazi za fasihi ya Kiswahili. Hali hii inasababisha tatizo katika kuzielewa kazi
mbalimbali za fasihi ya Kiswahili. Utafiti ulifanyika maktabani na uwandani.
Maktabani tuliyadurusu mapitio mbalimbali kama vile majarida, tasnifu, tahakiki,
makala na vitabu. Uwandani tulitumia mbinu ya udurusu wa maandiko, mahojiano
na ushuhudiaji. Mbinu hizi zilitusaidia katika kukusanya data mbalimbali
zinazohusiana na utafiti huu.
Maeneo ya Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Dodoma na Dar es Salaam yalitumika
katika ukusanyaji wa data. Utafiti huu ulitumia nadharia ya mwitiko wa msomaji au
wasikilizaji/hadhira ambayo ilitumika kwa kupata fikra binafsi za wasomaji na
wasikilizaji kutokana na uwelewa wao wa Kasida walizozisoma na kuziimba.
Uchambuzi wa data uliegemea katika maelezo kwa kuwa utafiti huu ni wa kitaamuli.
Hivyo, haukujihusisha na mwegamo wa kitakwimu.
Matokeo ya utafiti yanaonesha utanzia ni mbinu ya kibunilizi inayofungamana na
utanzu mkongwe wa Kasida za kitanzia ambazo ndani yake hutoa ujumbe na hisia
kwa wasomaji na wasikilizaji.
Description
Tasnifu (Shahada ya Uzamili katika Fasihi ya Kiswahili)
Keywords
Utanzia, Kasida za Kiswahili, Unguja, Kasida, Mjini Magharibi Unguja, Kiswahili, Zanzibar, Fasihi ya Kiswahili
Citation
Moh’d, H. K. (2016). Utanzia katika kasida za Kiswahili: Mifano kutoka mkoa wa Mjini Magharibi Unguja (Tasnifu shahada ya uzamili). Chuo Kikuu cha Dodoma, Dodoma.