Ufutuhi katika nyimbo za sherehe za unyago wa Wazaramo: utumizi na dhima zake kwa hadhira
Loading...
Date
2014
Authors
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
Chuo Kikuu cha Dodoma
Abstract
Utafiti huu ulichunguza ujitokezaji wa ufutuhi katika nyimbo za sherehe za unyago
wa Wazaramo kwa kuangalia utumizi na dhima zake kwa hadhira. Dhana ya ufutuhi
imefasiliwa kuwa ni hali furaha, ucheshi, kicheko au tabasamu itokanayo na vijenzi
mbalimbali. Vijenzi vya ufutuhi vilivyomakinikiwa katika utafiti huu ni kejeli,
vijembe, dhihaka, na balagha.
Utafiti ulifanyika uwandani na maktabani ambapo data za utafiti zilikusanywa na
baadaye kuchambuliwa na kuwasilishwa kwa njia ya ufafanuzi wa kimaelezo.
Maeneo yaliyotumika katika kukusanya data za utafiti yalikuwa ni mikoa ya Pwani,
Dar es salaam na Dodoma. Uchambuzi wa data ulizingatia misingi ya nadharia ya
Uhalisia ambayo ni; uhalisia kama mwelekeo, uhalisia kama mbinu ya kisanaa, na
uhalisia kama mbinu ya kihakiki. Nadharia hii ilisaidia kufafanua uwiano uliopo kati
ya sanaa ya uimbaji itumikayo katika sherehe za unyago wa Wazaramo na uhalisia
wa matukio ya kila siku yatokanayo na mfumo wa maisha ya jamii hii.
Matokeo ya utafiti huu yanaonesha kuwa hali ya utani, hofu na sababu za kihistoria
ndizo huwafanya Wazaramo watumie tungo za kifutuhi wakati wa sherehe za
unyago. Pia, matokeo yanabainisha kuwa Wazaramo hutumia ufutuhi katika nyimbo
za unyago wa kama kibebeo cha fikra, na hisia zinazolengwa kuwekwa wazi mbele
ya hadhira iliyokusanyika. Ufutuhi unaochopekwa katika tungo hizi huifanya hadhira
kuzing'amua na kuzielewa kwa njia iliyojaa ucheshi, kicheko, na tabasamu. Dhamira
hizi huweza kumhusu mwali wa Kizaramo anayefanyiwa unyago, mzazi au mlezi
wake pamoja na washiriki wengine waliokusanyika katika sherehe husika.
Description
Tasnifu (MA Kiswahili)
Keywords
Ufutuhi, Nyimbo, Unyago, Wazaramo, Dhima, Hadhira, Sherehe, Fasihi simulizi, Vijembe, Dhihaka, Balagha
Citation
Juma, S. (2014). Ufutuhi katika nyimbo za sherehe za unyago wa Wazaramo: utumizi na dhima zake kwa hadhira (Tasnifu). Chuo Kikuu cha Dodoma, Dodoma.